Jumatano, 7 Agosti 2013

Kuungana vyuo vikuu vya EAC, kutaokoa elimu?



Wakati suala la ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki(EAC) likiendelea kujadiliwa namna ya utekelezaji wa mambo mbalimbali ikiwamo sarafu moja na suala la kisiasa, Baraza la Elimu ya Vyuo Vikuu kwa ukanda huu(IUCEA) linataka taasisi zake zitoe elimu inayofanana.
Msukumo wa kutoa kiwango cha elimu kinachofanana, unatokana na hali iliyopo sasa kwa wahitimu wa vyuo vikuu katika nchi za EAC kushindwa kumudu ushindani wa soko la ajira duniani.
Katibu Mtendaji wa IUCEA, Profesa Mayunga Nkunya anasema mfumo huo utasaidia wahitimu wa jumuiya hiyo kupata taaluma itakayokuza mahitaji katika soko la ajira duniani.
Akizungumzia mfumo wa elimu wa Tanzania, Profesa Nkunya anasema ni wa kizamani ambao haimsaidii mwanafunzi anapohitimu masomo yake.
“Kwetu sisi mtihani ndiyo kigezo pekee cha kumpima mwanafunzi, kufanya hivyo ni kosa kwa sababu kunawengine wanafeli lakini wanauwezo mzuri tu kwenye masuala mengine. Tunataka kuwa na mfumo katika Afrika Mashariki unaoangalia uwezo wa kila mtu” anasema.
Anasema kama nchi hizo zitaendelea na mfumo wa sasa wa kuchukulia mtihani kuwa kipimo pekee cha kupima uelewa wa mwanafunzi, zitazidi kupoteza nafasi nyingi za watu wenye uwezo.
Profesa huyo anasema katika nchi za EAC ni Rwanda pekee ndiyo imebadili mfumo wake wa elimu ambao unatoa fursa kwa kila mtu kupata elimu bila kuhukumiwa na kigezo cha kufaulu au kutokufaulu kwenye mitihani.
Anaongeza kuwa nchi zilizoendelea duniani zimefanikiwa kutoa elimu kwa watu wake kwa sababu kwao mitihani siyo kigezo cha kupima uwezo wa mtu.
Akizungumzia mpango huo wa IUCEA Msemaji wa Tume ya Vyuo Vikuu hapa nchini (TCU), Edward Mkaku anasema haoni ubaya wowote wa mpango huo lakini IUCEA haina mamlaka katika vyuo vikuu vya Afrika Mashariki kwani kila nchi ina sheria zake katika suala la elimu.
Mkaku anasema ili hatua hiyo ifikiwe, inabidi kila nchi mwanachama wa EAC iafiki kujiunga na mpango.
Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Biashara la Afrika Mashariki (EABC), Andrew Kaggwa anasema anasema wahitimu wa elimu ya vyuo vikuu katika nchi za EAC, wana ujuzi mdogo ambao hauwezi kufanya vizuri kwenye soko la ushindani.
Kaggwa anasema mfumo huo wa elimu utasaidia EAC kutatua changamoto ya ajira kwa wahitimu wa elimu ya juu kutokana na kile alichoeleza kwamba wataweza kutengeneza bidhaa zao wenyewe badala ya kutegemea bidhaa kutoka nje. Mkurugenzi huyo anasema wataalamu kutoka Asia, China na Amerika ndiyo wamejaa katika nchi za EAC kwa sababu watu wa jumuiya hii wamekosa ujuzi unaowasaidia kumudu kuendesha viwanda na biashara katika nchi zao.
“Sisi tunawafanyia kazi wenzetu kwa kuwauzia malighafi ambazo wanazileta huku kama bidhaa na kutuuzia tena” anasema Kaggwa.
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) mkoani Morogoro, Eliaza Mkuna ambaye anasomea Shahada ya Uzamili wa Sayansi katika Kilimo na Uchumi, anasema licha ya mpango huo kuwa mzuri, tatizo lipo kwenye elimu ya chini.
“Jinsi tunavyomuandaa mwanafunzi kuanzia ngazi ya chini tunatofautina katika nchi hizi tano, ukizingatia Tanzania tumekumbwa na anguko la elimu kwa siku za hivi karibuni” anasema msomi huyo.
Anasema kuwa maandalizi ya kutosha yanahitajika kabla ya mpango huo kuanza kazi. Anasema maono ya kielimu katika nchi hizi yanatofautiana kutokana na kila moja kuwa na vipaumbele vyake.
“Tanzania tuna ‘Big Result Now’ je tunajua nchi nyingine zina dira gani? Je zinashabihiana?” anahoji Mkuna.
Anasema elimu inategemea vitu vingi ambavyo vinatofautiana kati ya nchi moja na nyingine ambapo anatolea mfano wa vitabu vinavyotumika kufundishia katika shule za Kenya ni tofauti na vile vinavyotumika nchini Tanzania.
Jarida la IUCEA la mwaka jana lilimnukuu Rais wa Rwanda, Paul Kagame akisema bado nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki hazijafikia lengo la Umoja wa Mataifa(UN) la kuwa na angalau asilimia 10 ya watu wenye elimu ya kiwango cha chuo kikuu.
Rais Kagame anasema kiwango kilichopo sasa cha asilimia tano hadi saba ni kidogo ukilinganisha na lengo la UN.
Kagame anawataka viongozi wa IUCEA kutekeleza mipango yao ya maendeleo na kuhakikisha kuwa vyuo vikuu vya EAC, vinashirikiana katika rasilimali walizonazo ili kufanikiwa kitaaluma na kitafiti.
Kagame aliongeza kuwa nchi yake na wanachama wengine wa EAC wanatarajia mipango yenye mashiko inayoakisi mafanikio ya kuwa na jumuiya ya Afrika Mashariki.
Katika kuhakikisha mchakato huo unatimia Kaggwa anasema, baraza hilo ambalo baadhi ya vipaumbele vyake ni pamoja na masuala ya weledi, uwajibikaji, usawa na ubunifu limeandaa kongamano litakolishirikisha wafanyabiashara, wataalamu na taasisi mbalimbali litakalofanyika jijini Nairobi mwezi Oktoba mwaka huu. Lengo la kongamano hilo litakuwa ni kukutanisha sekta za umma na binafsi ili kujadili namna ya kuboresha sekta ya elimu katika nchi za EAC.
Baraza hilo linalenga kuunda mtandao wa vyuo vikuu kwa nchi za ukanda wa Afrika Mashariki pamoja na vya nje ya jumuiya hiyo. Pia linalengo la kuunda jukwaa litakalokuwa linajadili masuala ya kitaaluma na mambo mengine yanayohusiana na elimu ya juu.