HATIMAYE ripoti ya Tume ya Haki za 
Binadamu na Utawala Bora, kuhusu vitendo vya uvunjaji wa haki za 
binadamu na mauaji yaliyotokea Arusha Januari 5, 2011 kwenye maandamano 
ya CHADEMA imevuja.
Licha ya ripoti hiyo kufichwa kwa 
kutosomwa hadharani kwenye vyombo vya habari kutokana na kulishutumu 
moja kwa moja Jeshi la Polisi, Tanzania Daima imefanikiwa kuinasa.
Maandamano hayo ya CHADEMA ya kupinga 
ukiukwaji wa kanuni na sheria katika uchaguzi wa Meya ya Manispaa ya 
Arusha, Gaudence Lyimo, licha ya kuruhusiwa na polisi awali baadaye 
yalipigwa marufuku na Mkuu wa Jeshi hilo nchini, IGP Saidi Mwema.
Hata hivyo, CHADEMA walikataa kutii 
agizo hilo kutokana na taarifa ya IGP kutowafikia kwa maandishi kama 
inavyoelekezwa kwa mujibu wa taratibu za utendaji wa jeshi hilo.
Kufuatia vurugu hizo za polisi na 
wafuasi wa CHADEMA, watu watatu waliuawa kwa kupigwa risasi, wengine 
zaidi yya 30 kujeruhiwa na wafuasi zaidi ya 70 wakiwemo viongozi 
waandamizi wa chama ambao walifunguliwa mashtaka mahakamani.
Kutokana na tukio hilo Tume ya Haki za 
Binadamu, iliunda tume iliyochunguza suala hilo Januari 10 hadi 13 mwaka
 2011, kwa kuwahoji viongozi wa CHADEMA mkoa wa Arusha, Jeshi la Polisi,
 hospitalini walipolazwa majeruhi na njiani walipoandamana wafuasi wa 
chama hicho.
Tume hiyo iliongozwa na Kamishna 
Joaquine De-Mello akiandamana na ofisa uchunguzi, Philipo Sungu, kutoka 
idara ya elimu kwa umma na mafunzo kufuatilia tukio hilo kwa muda wa 
siku tatu ili kupata picha halisi.
Lengo kuu lilikuwa kubaini chanzo cha 
vurugu hiyo, uvunjwaji wa haki za binadamu ambapo Januari 11, asubuhi 
tume hiyo ilianza kuonana na madaktari na wagonjwa majeruhi waliolazwa 
katika hospitali mbili za Mount Meru na Seliani.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo ambayo gazeti 
hili linayo nakala yake, taarifa zilizopatikana katika hospitali 
zilionyesha kupokelewa kwa majeruhi 26 katika hospitali ya Mount Meru na
 wawili Seliani.
Majeruhi watatu walipoteza maisha wakati
 wakipatiwa matibabu ya awali hapo hospitali ya Mount Meru, 22 walilazwa
 katika hospitali ya Mount Meru na watatu walipatiwa matibabu na 
kuruhusiwa kuondoka hospitalini.
Ripoti ya madaktari ilithibitisha kuwa 
vifo hivyo vilitokana na majeraha ya risasi za moto huku majeruhi 
wengine wakithibitisha kupigwa risasi za moto huku wakionyesha majeraha 
hayo kwenye miili yao.
Licha ya ripoti kuonyesha vitendo hivyo 
vya uvunjifu wa haki za binadamu uliofanywa na polisi, inasema kuwa 
maandamano ya CHADEMA na mkutano yalikuwa halali na jeshi ndilo 
lilisababisha fujo hizo kwa kutofuata sheria.
“Tanzania inajivunia Katiba inayoainisha
 vipengele mbalimbali vinavyotambua na kulinda haki za msingi za 
binadamu, hivyo kama nchi nyingine inawajibika kwa Azimio la Ulimwengu 
la Haki za Binadamu la mwaka 1948 (UDHR) ambalo ni mama wa matamko, 
makubaliano na mikataba ya vizazi vyote vya haki,” inasema ripoti hiyo.
Kwamba Tanzania kama miongoni mwa nchi 
wanachama zilizoweka sahihi na kuridhia mikataba hiyo zinawajibika moja 
kwa moja “kuheshimu, kulinda, kutetea na kutekeleza” haki zilizoainishwa
 kwenye mikataba husika.
Ripoti hiyo inaongeza kuwa “kanuni za 
jumla za jeshi la polisi namba 403 kifungu cha kwanza inasema; Mtu 
yeyote ambaye anataka kuitisha, kukusanya, kuandaa na mkutano wowote au 
maandamano katika eneo lolote hadharani atapaswa kuwasilisha taarifa ya 
maandishi si chini ya saa 48 kabla ya wakati mkutano au maandamano 
kufanyika kwa ofisa wa polisi wa wilaya husika.
Na pindi anapopelekea taarifa kwa 
maandishi kwa mkuu wa polisi wa wilaya anaruhusiwa kuendelea kuandaa, 
kuitisha, kukusanya, kuunda, au kuandaa mkutano au maandamano kama 
ilivyopangwa.
Ila mpaka atakapopata taarifa ya 
maandishi kutoka kwa Afisa Polisi wa Wilaya husika kueleza sababu za 
kusitisha maandamano hayo.”
Ripoti hiyo inasema kuwa kwa mujibu wa 
sheria hiyo, polisi “Officer in charge” wa eneo katika eneo hilo la 
Arusha mjini ni OCD wa Arusha Mjini – ndiye aliyepaswa kutoa maelekezo 
ya kuzuia maandamano na si Kamanda wa Polisi wa Mkoa au Inspekta 
Jenerali wa Polisi.
“Kwa mantiki hii, taarifa ya CHADEMA kwa
 polisi ilitosha kwa wao kuendelea na mipango yao ya maandamano na 
mkutano kama inavyoelezwa kisheria,” anasomeka taarifa hiyo.
Pia inaonyesha kuwa Sheria Na. tano (5) 
ya mwaka 1992 ya vyama vya siasa kifungu cha 11 vifungu vidogo vya (4) 
na (6) na sheria Na. 1 ya 1939 ya polisi na huduma za mgambo kifungu 
43.-(1), (2), zilikidhi pia hitaji la CHADEMA kuendelea na mipango yao 
ya maandamano na mkutano wa hadhara kama ilivyopangwa.
Kwamba Sheria Na.5, 1992 ya vyama vya 
siasa kifungu 11. — (8) inasema: kama jeshi la polisi linasitisha 
maandamano au mkutano taarifa hizo hutolewa kwa maandishi kueleza 
sababu, wala si kutumia televisheni, kama ilivyojitokeza kwa tukio la 
Arusha.
“Hivyo CHADEMA walikuwa sahihi kwa kuwa 
hawakupata taarifa ya kimaandishi licha ya polisi kudai kutoa barua hiyo
 lakini walishindwa kuthibitisha madai yao mbele ya tume.
Ripoti hiyo pia inaongeza kuwa askari 
walifanya vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji dhidi ya viongozi na 
waandamanaji hasa wanawake bila kujali hali zao.
Kwa mfano wanatajwa mbunge wa viti 
maalum Lucy Owenya na mke wa Katibu Mkuu wa CHADEMA, Josephine 
Mushumbusi, kuwa walipigwa na kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za 
miili yao.
Kwamba viongozi wa CHADEMA na wananchi wengi walikamatwa na kuwekwa rumande katika kituo kikuu cha polisi kati mjini Arusha.
“Askari waliwapiga waandishi wa habari, 
waliwanyang’anya vifaa vyao vya kazi na kufuta picha na kazi walizokuwa 
wanazifanya kwenye maandamano. Askari na waandamanaji walisababisha 
uharibifu wa magari na mali za umma na wananchi.
“Aidha walisababisha upotevu wa mali za 
wananchi zikiwemo simu mbili za mkononi za Owenya na fedha tasilimu sh 
2,700,000 za majeruhi Ally Ogaga walizodai kunyang’anywa na askari, 
wakati Ofisi ya CCM Mkoa wa Arusha ilivunjwa vioo kwa mawe na 
waandamanaji na nyumba ya mwananchi Salum Ally iliungua kwa moto 
uliosababishwa na mlipuko wa bomu lililoruka kutoka kwenye gari la 
polisi,” ilisomeka.
Tanzania Daima
