IMEBAINIKA kuwa baadhi ya maofisa wa 
polisi na makachero wao wamekuwa wanatumia vibaya majina ya viongozi 
wakuu wa serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kama kisingizio cha 
kupika kesi za ugaidi dhidi ya viongozi wakuu wa Chama cha Demokrasia na
 Maendeleo (CHADEMA).
Katika tukio la hivi karibuni, makada wa
 CHADEMA waliokuwa rumande wakikabiliwa na mashitaka ya ugaidi, ambayo 
hatimaye yalifutwa na mahakama, wametoboa siri kuwa miongoni mwa majina 
yaliyotumiwa na baadhi ya polisi na makachero waliowatesa ni ya Rais 
Jakaya Kikwete; na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, 
Sophia Simba.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati 
tofauti, wiki hii, makada hao - Evodius Justinian, Oscar Kaijage, Rajabu
 Kihawa, Seif Magesa na Henry Kileo, wamesema pia kuwa njama hizo za 
polisi na makachero wao, zililenga kuwalazimisha vijana hao wawahusishe 
viongozi wakuu wa CHADEMA (hasa Mwenyekiti, Freeman Mbowe na Katibu 
Mkuu, Dk. Willibrod Slaa) na ugaidi na utesaji watu ambao umekuwa 
unaendelea.
Wengine ambao polisi walitaka watajwe ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na Mbunge wa Ubungo, John Mnyika.
Hata hivyo, vijana hao wanasema waligoma kuwahusisha, hata baada ya kuteswa kikatili.
Makada hao wanadai kwamba mateso waliyopata yaliratibiwa na viongozi wa Jeshi la Polisi, Advocate Nyombi na afande Pasua.
Mmoja wa makada hao, Kihawa, 
aliyekamatwa na kupelekwa Kituo cha Polisi Dodoma, anadai kuwa alipokuwa
 anahojiwa, alilazimishwa aseme kuwa viongozi wa CHADEMA ndio wanahusika
 na utekaji na tindikali.
Akiendelea kusimulia mkasa huo, Kihawa 
alisema kuwa baada ya kauli hiyo, aliingizwa katika chumba namba 114, 
ghorofa ya pili, chenye kamera nyingi katika moja ya hoteli maarufu 
Mjini Dodoma (jina tunalihifadhi kwa sasa) akavuliwa nguo zote, 
akakalishwa kwenye chupa ya soda kisha akapigwa sana.
“Nilipoteza fahamu lakini nilipozinduka 
nilikuta nimevalishwa nguo, na nimekalishwa kwenye kiti na kuwekewa 
chakula karibu,” anasema, na kuongeza kuwa hakula chakula hicho, lakini 
alipotoka nje ya chumba hicho, kwenye ukumbi wa hoteli, aliwakuta vijana
 waliofukuzwa CHADEMA, Juliana Shonza na Mtela Mwampamba na Habib 
Mchange wakinywa na kula.
“Walinikejeli sana, wakasema wanashangilia ushindi,” alisema.
Kutoka pale nilichukuliwa na Mbunge wa 
Maswa Magharibi, John Shibuda, akaniingiza chumbani akadai anampigia 
simu Waziri Simba, akamwambia, “mama, huyu kijana ninaye hapa. Ungeongea
 naye ili akubali kulegeza msimamo, au umpigie mwanao Jakaya anipigie, 
pengine atabadili msimamo wake kama tulivyokuwa tumekubaliana awali.”
Kihawa anadai kuwa mtu huyo aliyedaiwa 
kuwa Waziri Simba alimjibu Shibuda kuwa asingeweza kuzungumza yeye kwa 
kuwa alikuwa hajisikii vema, ila kwa suala la kuongea na Rais Kikwete, 
atafutwe Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana au Naibu Katibu 
Mkuu Bara, Mwigulu Nchemba, ili awaunganishe Shibuda na rais.
Kwa mujibu wa Kihawa, baada ya kupewa 
ushauri huo, Shibuda alijibu: “Mwigulu ni mropokaji, hawezi kuingizwa 
katika mkakati huu; na Kinana ni mgumu kuingilika katika suala hili.”
Anasema alisikia mazungumzo yao kwenye 
loud speaker ya simu ya Shibuda, na baada ya kukata simu Shibuda 
alimwambia kuwa alikuwa anazungumza na Simba, ambaye alidai ni ‘mama 
mdogo wa Kikwete.’
Kihawa anasema wakati anahojiwa hayo hapo hotelini, maofisa wa polisi walisimama kwa mbali wakimsubiri.
Wengine waliokuwapo wakishuhudia 
mahojiano hayo ni Meya wa Ilemela, Henry Matata na aliyekuwa Diwani wa 
Igoma, Adam Chagulani. Matata na Chagulani walishavuliwa uanachama na 
CHADEMA.
Wahusika walipohojiwa na Tanzania Daima jana, kila mmoja alikuwa na kauli yake kama ifuatavyo:
Tanzania Daima Jumapili: Afande Nyombi, 
vijana waliokuwa wametuhumiwa kwa kesi ya ugaidi kule Tabora, wamekutaja
 wewe kuwa ulishiriki kuwatesa ukiwalazimisha wawataje viongozi wakuu wa
 CHADEMA kuwa walishiriki kutenda ugaidi na utekaji. Unatoa ufafanuzi 
gani?
Advocate Nyombi: Mimi si msemaji wa Jeshi la Polisi, siwezi kusema chochote.
Tanzania Daima Jumapili: Msemaji 
atajuaje kama mliwatesa watu wakati wa mahojiano? Mbona huku ni kumwonea
 msemaji wa Jeshi la Polisi kusemea kila kitu hata mambo ambayo askari 
fulani ametenda kwa utashi wake?
Advocate Nyombi: Nimekwambia mtafute, msemaji katika hayo yote. Mimi siwezi kuongelea suala hilo, nakutakia Idd Mubaraka njema.
Tanzania Daima Jumapili: Afande Pasua, 
vijana waliotuhumiwa katika kesi ya ugaidi kule Tabora wamekutaja wewe 
kuwa ulishiriki kuwatesa, ukiwalazimisha wataje viongozi wa CHADEMA kuwa
 walishiriki kutenda ugaidi na utekaji. Unatoa ufafanuzi gani?
Afande Pasua: Kwani wewe uko wapi?
Tanzania Daima Jumapili: Nipo Dar es Salaam, hapa ofisini.
Afande Pasua: Njoo ofisini tuongee tuyaweke sawa unayouliza. Umesema unatoka gazeti gani?
Tanzania Daima Jumapili: Nimekwambia Tanzania Daima.
Afande Pasua: Mashtaka hayo kwanza 
yalikuwa ya serikali, mimi sifanyi kazi ya kubahatisha, mpigie msemaji 
wa Jeshi la Polisi mimi si msemaji. Alikata simu.
Henry Matata
Tanzania Daima Jumapili: Mstahiki Meya, 
vijana waliokuwa wanakabiliwa na kesi ya ugaidi wanadai walihojiwa mbele
 yako Dodoma. Je, unafahamu nini kuhusu suala hili?
Matata: Kijana Rajab Kihawa ndio 
namfahamu. Huyu alikuwa mfanyakazi wangu, ila tangu aache kufanya kazi 
hapa sijaonana naye. Lakini mimi nina ugomvi na wafanyakazi wote wa 
gazeti lenu na gazeti lenu. Nisingependa kuongea na nyie. Tangu 
nifukuzwe CHADEMA gazeti lenu linaongeza chumvi habari zinazonihusu. 
Mimi si meya kwa kura za CHADEMA. CHADEMA walinifukuza, CCM wakaona 
nafaa, wakanipa kura nikawa meya.
Tanzania Daima Jumapili: Ulikutana na Rajab Dodoma hotelini?
Matata: Nimekwambia sitaki kuongea na gazeti lenu.
bi Mheshimiwa, vijana waliokuwa 
wanakabiliwa na kesi ya ugaidi wamekutaja kuwa ulikuwepo wakati 
wanahojiwa Dodoma. Je, una kauli gani kwa yao hii?
Chagulani: Mimi nilikuwa Dodoma mwezi wa
 nne lakini nilikuwa Kondoa kwa ajili ya uhamisho wa mke wangu. Hayo 
unayonieleza siyajui.
Waziri Simba hakupokea simu, na alipotumiwa ujumbe mfupi wa simu hakujibu lolote.
Msemaji wa jeshi la Polisi, Advera 
Senso, alipoulizwa kama jeshi ndilo linawatuma polisi kutesa watu wakati
 linawahoji, alisema: “Mhalifu asitafute huruma ya jamii kwa kuzushia 
jeshi kwa uhalifu alioutenda yeye, na endapo ikibainika anasingizia 
uongo na hilo ni kosa pia, kwani Jeshi la Polisi linafuata taratibu za 
sheria.”
Shibuda alipoulizwa jinsi alivyohusika 
katika sakata hilo alisema kuwa kwa sasa hawezi kuzungumza chochote kwa 
kuwa alikuwa Agha Khan Hospitali akihangaikia mgonjwa wake.
“Niacheni kwa sasa kwa kuwa nahitaji 
utulivu wa akili niweze kushughulikia afya ya mgonjwa wangu. Nadhani 
hata kama ni wewe sijui katika mazingira kama haya ungeweza kweli 
kuongea?” alisema.
Msemaji wa Ikulu, Salva Rweyemamu, 
alipopigiwa simu kuulizwa ikiwa wanayo taarifa ya watu wanaotumia vibaya
 jina la rais katika matukio ya kihalifu aliomba jambo lolote 
linalohusiana na kazi, lisubiri kwa kuwa alikuwa katika mapumziko ya 
sikukuu.
“Ndugu yangu, unajua leo ni sikukuu na 
ni usiku, nitafute wakati mwingine, maana siwezi kuzungumzia mambo ya 
watu wa CHADEMA muda huu. Niache nipumzike kidogo halafu tuwasiliane 
siku ya kazi,” alisema
