Serikali ya Rwanda imetoa tamko 
linaloonyesha kutoielewa kauli ya Rais Jakaya Kikwete, iliyoamuru 
wahamiaji haramu kuondoka nchini, hali inayoonekana kukwepesha hoja. 
Rwanda kupitia waziri wake wa Mambo ya 
Nje, Louise Mushikiwabo, ilikaririwa ikieleza kwamba hawatajibu mapigo 
agizo la Rais Jakaya Kikwete ya kuwataka Wanyarwanda wote waliolowea 
Magharibi mwa Tanzania kuondoka haraka.
Mushikiwabo alisema wako tayari 
kuwapokea na kuwalinda wote waliofukuzwa Tanzania kwa kisingizio kuwa ni
 wahamiaji haramu, akieleza kwamba anasikitishwa kwa kuwa Tanzania 
haikufanya jitihada yoyote kuwasiliana na Rwanda kuhusu suala hilo kabla
 ya kuchukua uamuzi huo.
“Ni uamuzi ambao umeshachukuliwa, 
hatukushirikishwa kwa namna yoyote na jukumu letu kama serikali na taifa
 ni kuwahakikishia ulinzi wote wanaokuja, na hili ndilo suala 
tunalolishughulikia kwa sasa,” alisema.
Kwa mujibu wa gazeti la New Times, 
Mushikiwabo aliwaeleza waandishi wa habari kwamba agizo hilo la Rais 
Kikwete pamoja na ushauri wa kuitaka Serikali ya Rwanda kuzungumza na 
wanamgambo hasimu wa FDLR waliopo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo 
(DRC), hayatayumbisha uhusiano imara baina ya Watanzania na Wanyarwanda.
“Sisi si majirani tu, tuna mfungamano 
imara baina ya watu wetu pia, tuna mfungamano wa damu, wa kibiashara, na
 mengine mengi ya kutufanya tuendelee kuwa pamoja,” alisema na kutumia 
fursa hiyo kuwakaribisha Watanzania nchini Rwanda.
Watanzania wanaweza kuishi hapa kwa umri
 wowote wanaotaka. Tunawachukulia kuwa ni watu wetu muhimu kwenye 
fungamano la Jumuiya ya Afrika Mashariki,” alisisitiza.
Rais Kikwete wakati akihitimisha ziara 
yake mkoani Kagera alitoa agizo la kuwataka wanaomiliki silaha kinyume 
cha sheria na wahamiaji haramu ama kuondoka au kuhalalisha ukazi wao, 
huku akitoa wiki mbili kwa zoezi hilo kutekelezwa, kabla ya kuanza kwa 
operesheni ya kuwasaka watu hao.
Kauli hiyo ilitokana na kushamiri 
vitendo vya kihalifu katika eneo la Kanda ya Ziwa, Rais hakutaja jina la
 nchi ya wahamiaji hao. Kwa ukanda huo Tanzania inapakana na Kenya, 
Uganda, Rwanda, Burundi na DRC.
Pia, Rais Kikwete katika hotuba yake ya 
mwisho wa mwezi alizungumzia kusikitishwa na kauli za shutuma, kejeli na
 udhalilishaji zilizotolewa na Rais Paul Kagame wa Rwanda dhidi yake.
Mvutano baina ya Rwanda na Tanzania 
ulianza kuwekwa hadharani Mei mwaka huu, baada ya Rais Kikwete kuishauri
 Rwanda kukaa na kuzungumza na FDLR wenye makao yao DRC, hatua ambayo 
haikuifurahisha Serikali ya Rwanda.
Wakati Rwanda ikieleza hayo jana Katibu 
Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue alizungumza na gazeti hili, na kutaka majibu
 ya kauli hiyo ya Rwanda yatolewe na Wizara ya Mambo ya Nje na 
Ushirikiano wa Kimataifa.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje, 
Mkumbwa Ally alisema kauli iliyotolewa na Rais Kikwete ilikuwa ni 
ushauri, kwamba Rwanda wanaweza kuukubali ama la.
“Kilichomkasirisha Rais Kikwete ni lugha
 za matusi zilizokuwa zikitolewa na viongozi wa Rwanda, ila kwa hicho 
walichokisema sidhani kama kitakuwa na tatizo kwetu,” alisema Mkumbwa.
Alifafanua kwamba, alipokuwa mkoani 
Kagera Rais Kikwete hakutoa agizo la Wanyarwanda kufukuzwa, bali alitoa 
agizo la kuanza kwa operesheni ya kuwakamata wahamiaji haramu, wale 
wanaomiliki silaha kinyume na taratibu.
“Rais alizungumzia masuala ya jinai ‘Criminal Element’, siyo kuwafukuza Wanyarwanda,” alisisitiza.
Hatutazungumza na FDLR
Waziri wa Mambo ya Nje, Louise 
Mushikiwabo, aliendelea kusema sera ya Rwanda kuhusiana na makundi ya 
aina hiyo, iko wazi na haitabadilika, kauli ambayo amekuwa akiirudia 
kila mara na kuwataka wote wanaofikiria kuhusu Rwanda kuzungumza na FDLR
 kwa namna yoyote kusahau wazo hilo.
“Kama umehusika kwa namna yoyote na 
maangamizi, wewe utakuwa adui wa kila mtu. Ni wazi kwamba Wanyarwanda 
wote watakuwa kwenye majonzi iwapo kwa namna yoyote kutakuwa na 
mawasiliano ya FDLR,” alifafanua.
Kundi la FDLR ambalo ni kifupisho cha 
Democratic Forces for the Liberation of Rwanda, linaundwa na watu 
walioshiriki kwenye mauaji ya kimbari yaliyowalenga watu wa kabila la 
Watutsi mwaka 1994, na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 800,000 kwa 
miezi mitatu.
Kundi hilo ambalo limeweka makazi yake 
mashariki mwa DRC, linadaiwa kufanya mashambulizi kadhaa yakiwamo ya 
milipuko ya mabomu nchini Rwanda, ambapo mwezi uliopita shambulio la 
aina hiyo mjini Kigali lilisababisha vifo vya watu watatu na kujeruhi 
watu kadhaa.
Uhusiano wa kihistoria
Familia za Rwanda zikiwamo zilizoishi 
Tanzania tangu miaka ya 1950, zimeelezwa kuwa zimekuwa zikiwasili nchini
 humo kupitia mpaka wa Rusumo baada ya agizo la Rais Kikwete kuwataka 
wawe wameondoka ndani ya wiki mbili, kabla ya kuanza kwa operesheni 
rasmi ya kuwaondoa.
Kwa mujibu wa mamlaka nchini Rwanda, 
mamia ya Wanyarwanda waliokuwa wakiishi mkoani Kagera ambako ndiko 
Tanzania inapopakana na Rwanda wamekuwa wakirejea kwa wingi, ambapo hadi
 juzi, zaidi ya watu 300 walikuwa wameshaorodheshwa kwenye ofisi za 
Uhamiaji.
-Mwananchi
