WAZIRI wa Uchukuzi, Dk Harrison 
Mwakyembe, ameanza kufanya ziara ya kushitukiza jana saa 10 alfajiri 
katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), 
kuangalia mwenendo mzima wa usafirishaji wa mizigo.
Katika ziara hiyo alitembelea vitengo 
mbalimbali, kikiwemo cha ukaguzi wa mizigo na abiria pamoja na kitengo 
cha kamera, ambako hivi karibuni kulipita dawa za kulevya za mabilioni.
Dk Mwakyembe amefanya ziara hiyo siku 
tatu baada ya kuahidi kuhakikisha inawatia mbaroni watu wanaojihusisha 
na usafirishaji wa dawa za kulevya kupitia viwanja vya ndege, kikiwemo 
hicho chenye jina la Baba wa Taifa.
Meneja wa Usalama wa wanjani huo, 
Clemence Jingu, alikiri Dk Mwakyembe kufanya ziara hiyo ya kushitukiza, 
ambapo alioneshwa maeneo pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa 
uwanjani hapo wakati wa ukaguzi wa mizigo.
Mtoa habari wetu alisema Dk Mwakyembe, alitembelea eneo ambalo dawa za kulevya zilipita na kukamatiwa nchini Afrika Kusini.
Alisema Dk Mwakyembe aliona hali ya 
ukaguzi katika eneo hilo ilivyokuwa, na kubaini dawa hizo zilionekana 
katika mizigo lakini kulikuwa na uzembe au njama zilizotokana na maofisa
 waliokuwa wakikagua.
Kwa mujibu wa mtoa habari huyo, Dk 
Mwakyembe alipita katika eneo hilo, ambalo lilikuwa na ofisa wa Polisi 
ambapo alielezwa kuwa siku hiyo mbwa wanaotumika kubaini dawa hizo, 
walicheleweshwa kufika.
Dawa hizo za kulevya aina ya Crystal 
Methamphetamine zenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 6.8, zilikamatwa 
nchini Afrika Kusini hivi karibuni wakati zikisafirishwa kutoka 
Tanzania.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana 
kutoka nchini humo, wanawake wawili walikamatwa katika Uwanja wa Ndege 
wa Kimataifa wa Oliver Tambo, Afrika Kusini, wakitokea Tanzania.
Wanawake hao walikamatwa wakiwa na 
mabegi sita ambayo yalipokaguliwa yalikutwa na kilo 150 za dawa hizo, 
ambazo pia zinajulikana kama ‘Tik’.
Akitoa ahadi ya kukabiliana na biashara 
hiyo wiki hii, Dk Mwakyembe amesema anajitoa mhanga kuhakikisha Wizara 
yake inawatia mbaroni watu wanaojihusisha na usafirishaji wa dawa za 
kulevya, kupitia uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere.
“Nitajitoa mhanga juu ya biashara hiyo 
na siogopi vitisho vya watu, maana mimi nilishakufa siku nyingi, 
hatuwezi kuidhalilisha nchi yetu kiasi hicho.
“Dawa za kulevya sasa zinasafirishwa 
kupitia kiwanja cha ndege, ambacho kimepewa jina la mtu muhimu katika 
nchi yetu, Mwalimu Nyerere, ni aibu kwa nchi yetu na Taifa letu, kuona 
uwanja huo unatumika kwa biashara hiyo, nipeni muda, mimi ndiye Waziri 
wa Uchukuzi, hatutakubali hali hii,” alisema na kuongeza: “Pale uwanjani
 kuna ofisi nne, Polisi, Uhamiaji, Usalama wa Taifa na watu wa Mamlaka 
ya Viwanja vya Ndege, wote nimewaagiza wanipe taarifa, walikuwa 
wanafanya nini hadi dawa hizo zinapita uwanjani hapo?”
Alisema anawapa notisi watu wote 
wanaosafirisha dawa za kulevya kupitia uwanjani hapo, watambue kuwa 
alishajitoa mhanga kupambana na dawa za kulevya, maana ni biashara 
inayodhalilisha Taifa.
